LATEST NEWS

Thursday, May 17, 2018

Naibu Spika amzuia Waziri Mkuu kujibu maswali ya wabunge wa Chadema

Wabunge wawili wa Chadema leo Mei 17, 2018 wamejikuta njia panda baada ya Naibu Spika, Dk Tulia Ackson kumzuia Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kujibu maswali yao kwa madai kuwa si ya kisera.

Waliomuuliza Waziri Mkuu maswali bungeni leo katika kipindi cha maswali ya papo kwa hapo kiongozi huyo wa shughuli za Serikali bungeni ni mbunge wa Tunduma, Frank Mwakajoka , Pauline Gekul (Babati Mjini).

Gekul alimuuliza Waziri Mkuu kuhusu sera ya Serikali ya mwaka 1996 ya kushusha madaraka katika halmashauri na lengo likiwa ni kuzipa halmashauri nguvu, kubuni vyanzo vya mapato na kutumia.

“Stendi ya mabasi ya babati ilipokonywa kwa madai kuwa ni agizo la Rais na Rais amesema hahusiki bali ni viongozi wa Manyara, nini kauli ya serikali,” amehoji Gekul.

Baada ya swali hilo, Dk Tulia amesema si la kisera na linaweza kujibiwa na waziri hivyo kumtaka kukaa na kutafuta swali jingine.

Hata pale Gekul alipopewa fursa ya kuuliza jingine bado amesema ,”ni swali la kisera, “ jambo lililomfanya Dk Tulia kumtaka aketi.

Kwa upande wake Mwakajoka amesema kumekuwa na migogoro katika halmashauri mbalimbali nchini kati ya wakuu wa wilaya na madiwani, kutolea mfano Gairo, Malinyi na Mbeya Mjini.


Amesema katika Halmashauri ya Tunduma kuna mgogoro ambao umesababisha baraza la madiwani kutokaa kikao tangu Agosti 2017, kwamba licha ya maelekezo kadhaa ya waziri ila mkuu wa mkoa na wilaya wanagoma kufanyika kwa kikao hicho.

Kama ilivyokuwa kwa Gekul, Dk Tulia pia alipangua swali hilo na kubainisha kuwa linaweza kujibiwa na waziri mwenye dhamana.

Mara baada ya kipindi cha maswali na majibu kumalizika, Gekul amesimama kuomba mwongozo akitumia kanuni ya 68(7) akizungumzia swali lake lilizozuiwa akisema ni swali la kisera, “Lakini lina maslahi kwa umma kwa watu wa Babati na Naibu Spika hili swali limekwisha kufikishwa kwa Waziri Mkuu na nyaraka tulishampatia, hili jambo limekuwa likisingiziwa Rais.”

“Waziri Mkuu ni msimamizi wa shughuli za Serikali na Rais kajivua hahusiki na mimi nimeuliza, nashindwa kuelewa, wabunge wengine wanauliza suala la jimboni na anajibiwa, nikuombe mwongozo wako, suala hili litaendelea hadi lini na suala la dhuruma mwisho hukurudia. Kwa nini meza isimwache waziri mkuu ajibu maswali yetu badala ya kumchagulia?”

Akijibu mwongozo huo, Dk Tulia amesema utaratibu waliojiwekea, kwamba maswali atakayoulizwa Waziri Mkuu yana utaratibu wake na ya mawaziri yana nafasi yake, “kama waziri mkuu analijua au halijui hilo si lenye mamlaka yangu.”

“Maswali ya majimbo yanaulizwa kwa mawaziri, maswali ya kisera ambayo mawaziri hawawezi kujibu ndio anaulizwa Waziri Mkuu. Kanuni zetu zimesema wazi maswali ya kisera au ya kijamii, kijamii si barabara ya jimbo lako.”

Amesisitiza, “ Si swali la Gekul pekee hata la Mwakajoka limezuiwa, swali la Tunduma waziri mkuu analijuaje. Niwasihi maswali kwa Waziri Mkuu tujielekeze katika maswali ya kisera.”

No comments:

Post a Comment

Adbox